Dhamana za uwekezaji zinavyoweza kukuongezea kipato Tanzania

Sep 17, 2015


Utamaduni wa kuhifadhi fedha benki na taasisi zingine za kifedha, unaongezeka taratibu kwa watanzania siku hadi siku.

Hii inafanyika kwa ajili ya usalama wa fedha zao na kupata faida inayotokana na riba toka  taasisi za kifedha.
Kwa mujibu wa  Ripoti ya Utafiti ya Mwaka 2013 uliofanywa na FinScope na kuzinduliwa Aprili mwaka jana na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania ( BOT ) Prof. Benno Ndulu, inaonyesha Watanzania milioni 3.3 wanatumia huduma za kibenki. 


Utafiti pia umeonyesha ongezeko la Watanzania milioni 12 wanaotumia huduma za kifedha zisizo rasmi, katika kipindi cha miaka minne iliyopita  hadi kufikia mwaka jana.
Pia umeonyesha  upande mwingine kuwa, ile hali ya kuhifadhi fedha majumbani kwa baadhi ya watu bado ipo.

Asilimia 70 ya Watanzania kwa mujibu wa utafiti hu, bado wanatunza fedha zao nyumbani badala ya kwenye mfumo rasmi, yaani ule wa benki na huduma nyingine za kifedha.
Pia unabainisha kwamba, asilimia 70.4 ya Watanzania milioni 24.2 wanaostahili kupata huduma za kifedha, hawazitumii kutokana na sababu mbalimbali.

Utafiti huo uliosimamiwa na Mfuko wa Kuendeleza Sekta ya Fedha Tanzania (FSDT), ulilenga kujua idadi ya Watanzania wanaofikiwa na kutumia huduma za kifedha, na namna wanavyozitumia nchini.

Pamoja na uwapo wa ongezeko la wananchi wanaotumia huduma za kibenki na za taasisi zingine za kifedha kwa ajili ya kuboresha maisha yao kama zilivyoonyeshwa kwenye utafiti huo, bado kuna eneo ambalo halijachangamkiwa vya kutosha na wananchi.


Eneo hili  kimsingi ni salama, la uhakika na lenye kuinua hali za kipato cha wananchi na taifa kwa ujumla, ni lile la kuwekeza au kuhifadhi fedha zao kwenye dhamana za serikali za muda mfupi (Treasury bills) na za muda mrefu (Treasury bonds).

Akizungumza kwenye semina ya waandishi wa habari iliyofanyika  Bagamoyo kuhusu dhamana za serikali za muda mfupi na za muda mrefu, Mkurugenzi Mshiriki wa Kurugenzi ya Masoko wa BOT Paul Maganga alisema,  eneo hilo liko wazi kwa Watanzania wote. Maganga alisema, uwekezaji huo unawafaa watu wa kada zote kuanzia wakulima wa kawaida, wastaafu, vyama vya ushirika, Saccos na wengineo wenye kiasi kinachokubalika kuwekeza.

“Kiwango cha chini cha kushiriki kwenye uwekezaji huu ni Sh.500,000 kwa dhamana za serikali za muda mfupi na Sh. 1,000,000 kwa dhamana za serikali za muda mrefu,” alisema.
 Maganga alisema kuwa, uwekezaji huo unawafaa watu wote wenye shughuli zao za kila siku  ama za msimu, kama vile wakulima na wastaafu.

Alisema uwekezaji huu unawafaa wakulima wanapokuwa wameuza mazao yao, ama wastaafu wanaopata fedha zao kwa kipindi fulani fulani, kama vile baada ya kila miezi mitatu.
Maganga alisema, kuna tija kwa kada hii ya wananchi kuwekeza fedha zao zitokanazo na mauzo ya mazao yao, ama kiinua mgongo na pensheni zao kwenye dhamana za serikali za muda mfupi ama mrefu, kwani zitawasaidia kuishi maisha yenye mafanikio.

Ofisa Mkuu wa BOT Mohamed Kailwa  akifafanua kuhusu  dhamana za serikali alisema ni nyenzo inayotumiwa na serikali kukopa kutoka kwa wananchi wake.
“Serikali inakopa kutoka kwa wananchi kwa ajili ya kupata fedha za kugharamia utekelezaji wa miradi yake mbalimbali ya maendeleo, kwa ahadi ya kuzirudisha na riba baada ya kipindi fulani, kiwe cha muda mfupi (Treasury bills) ama cha muda mrefu na za muda mrefu (Treasury bonds),” alisema.

                               

Kailwa alisema kuwa, serikali inakopa kupitia  masoko ya fedha ambayo dhamana za serikali huuzwa kwa njia ya mnada unaoendeshwa na BOT. 
Masoko ya fedha  alisema kuwa, ni kama yalivyo masoko mengine ya kawaida tofauti ni kwamba katika masoko haya, bidhaa kuu inayouzwa ni fedha.


Kailwa alisema, ununuzi wa dhamana za serikali za muda mfupi hufanywa kwa njia ya mnada unaoendeshwa na BOT kila wiki siku ya Jumatano
 “ Mwananchi anaweza kununua dhamana za serikali za muda mfupi unaohusisha siku 35, 91, 182, na 364.” Alisema.
Mwananchi mwenye kiwango kinachoanzia Sh. 500, 000 na kuendelea, alisema kuwa anaweza kununua dhamana  za muda mfupi kwa kuchagua siku anazotaka kuikopa serikali kati ya zilizotajwa hapo juu.

“Dhamana za serikali za muda mfupi zinauzwa kwa punguzo kwa kila Sh. 100, kwa maana kwamba mwekezaji anapoikopesha serikali kwa mfano Sh.95 kwa kila 100,  atalipwa zote sh. 100 baada ya kuiva kwa muda wa siku alizochagua,” alisema. Matokeo ya mnada hutolewa siku hiyo hiyo ya mnada kupitia tovuti ya BOT au kwenye ofisi zote za mawakala walioidhinishwa na benki hiyo.
Alisema serikali huwalipa walionunua  dhamana hizo za fedha na riba zao, baada ya kuiva kwa kipindi cha dhamana husika.

Kwa upande wa dhamana za serikali za muda mrefu, Kailwa alisema kuwa, hulipwa mara mbili kwa mwaka.
“Kiwango cha fedha cha chini kuwekeza katika dhamana hizi za muda mrefu, huwa ni sh. milioni moja na kuendelea, kwa muda wa miaka miwili, mitano, saba, 10 na 15,” alisema
Aidha alisema, viwango vya riba ya dhamana za muda mrefu huwa ni asilimia 7.82 kwa mwaka kwa dhamana ya miaka miwili, asilimia 9.18 kwa mwaka kwa ile ya miaka mitano, asilimia 10.08 kwa mwaka kwa ile ya miaka saba, asilimia 11.44 kwa mwaka kwa ile ya miaka 10 na asilimia 13.50 kwa mwaka kwa ile ya miaka 15.

“ Ninawaasa Watanzania kutumia kwa ukamilifu fursa hii ambayo bado haijafahamika na wengi ili kujiletea maendeleo yao binafsi, na kukuza uchumi wa nchi,” alisema na kuendelea.
“Kabla ya kushiriki katika mnada, mwekezaji yeyote anapaswa kufungua akaunti ya dhamana za serikali kwa wakala atakayemchagua na kujaza fomu maalumu ya zabuni toka kwa mawakala maalumu waliosajiriwa na BOT, ambao wako katika maeneo mbalimbali nchini,” alisema

Alisema, mawakala hawa wameidhinishwa kushiriki kwenye minada moja kwa moja kwa niaba yao wenyewe,  pia kwa niaba ya wateja wao.
Kailwa alisema, BOT hutoa tangazo la mnada kupitia vyombo vya habari kila siku ya Ijumaa na mawakala hujaza maelezo ya fomu kwenye mfumo maalumu wa benki hiyo uitwao Central Depository System (CDS).
Alisema mfumo huu, hufanya mchakato na kutunza kumbukumbu za minada kielektroniki.

Kuhusu malipo kwa dhamana zilizonunuliwa na wananchi, Kailwa alisema, muda wa kuiva dhamana za muda mfupi utakapowadia, wawekezaji watalipwa asilimia 100 ya thamani ya dhamana ikiwa imejumuishwa na thamani ya manunuzi na faida.

“Kwa upande wa wawekezaji wa dhamana za serikali za muda mrefu, wawekezaji watalipwa faida mara mbili kwa mwaka, na faida itategemea kiwango cha riba kilichowekwa kwa kila dhamana,” alisema na kuendelea.

“Kwanza ni salama kwa mwananchi, serikali haitarajiwi kushindwa kulipa wadai wake  dhamana zinapoiva. 
Mwekezaji anaweza kuziuza kabla ya muda wake wa kuiva kama itakuwa lazima kufanya hivyo,” alisema.
Maganga alifafanua faida nyingine kwa dhamana hizo za serikali kutolewa kama dhamana kwa ajili ya mikopo.

“Ni wakati muafaka sasa kwa wananchi wa kada zote kuchangamkia fursa hii kwa minajili ya kuboresha maisha yao na kustawisha uchumi wa nchi kama wananchi wa mataifa mengine wanavyofanya,” alisema

Source: Nipashe
Share on :
 
Copyright © 2015 Raizoni Blog
Distributed By My Blogger Themes | Design By SPARTO Inc Team