Aliomba fedha aliponyimwa, akamtukana mwenye duka...

Feb 11, 2015


Mwandishi Freddy Macha

Sehemu ya magharibi ya London siyo sawa na ya Afrika Mashariki. Majira yanapobadilika na mwangaza wa jua kutumbukia;  huja na mbwembwe zake. Tuko msimu wa baridi kali yenye barafu  ukanda wa kaskazini wa dunia. Kiza huanza kukonyeza saa tisa alasiri. Hiyo saa kumi na moja jioni tunayosimuliana giza finyu lilishapiga deki. Mchana, kwaheri.
Lakini shughuli za wanadamu zilezile. Maduka hayajafungwa. Duka tunalotazama ni la hawa wamachinga pembe ya barabara kuu. Wahindi wenye maduka wanajuana kwa vilemba. Mmachinga wetu ni  Mpakistani. Ana kameza kake kadogo mbele ya upenu wa mita tano kwa mapana ya mita moja, kajaza simu za mkononi, vibiriti, sigara.  Jambo la ziada ni simu na vipengele vyake. Betri, waya, mikebe ya kuzifungia; kila unachokililia kwa simu yako;  ongeza yeye fundi.
Iko siku aliniambia kwao alihitimu ualimu ila sababu ya rabsha za kisiasa akatupilia mbali taaluma yake akafuata ndugu aliowajua  London. Ukimchunguza hajafikisha miaka ishirini na tano. Yuko hapa miaka miwili. Alianza kaduka bila meza na mifuko ya plastiki. Akiuza kadi za Lyca Mobile, kampuni ya bei rahisi inayotumiwa sana na wageni  Uzunguni. Mtanzania anapopiga simu kutoka huku mara nyingi anatumia mtandao wa Lyca.  Simu za viganjani ni biashara nzuri. Tuseme suala zima la kompyuta na mitandao ni kitengo chenye masilahi.
Watazameni vijana wawili waliounda WhatsApp. Mmoja kwao ni Ukraine. Walianza kitu kidogo tu lakini leo mabilionea  baada ya kumuuzia Myahudi anayemiliki Facebook uvumbuzi wao.  Vijana wa Kitanzania mnaosoma kuweni wabunifu. Jaribuni kutafiti na kujua nini kinatakiwa. Uchunguzi wa kina badala ya  domo sana na siasa za malalamiko.
Basi, Mpakistani alichangamkia umachinga na hizo kadi.  Baada ya miaka miwili, hauzi tu vidato vya simu. Anazikarabati. Ukimuuliza kajuaje, atakwambia alipofika  Uingereza alikwenda chuo akasomea ufundi  miezi kumi. “Mengine ni utundu tu...” Kaduka hakiishi wateja. Hula hapo hapo,  kutwa, kasimama akichora  fedha.
Siku hii tunayohadithiana nilitaka asafishe mfereji wa simu yangu uliokuwa na mushkeli. Wakati nimetoa pochi  n’namlipa paundi tano alizotaka (kama shilingi elfu kumi na mbili); kando yangu kajipachika bonge la mtu. Mwamba. Niliisikia sauti yake nzito kabla ya kushuhudia tambo lake. Macho yanakodolea zile fedha ninazomlipa Mpakistani.
“Nipe paundi moja nikanunue maji. Nitakurudishia.”
Kamngurumia Mmachinga. Sauti nzito.  Ilinikumbusha mchezaji fulani wa sinema. Nilipogeuka nikamaizi nimemfikia begani. Mweusi sana. Hajavaa nguo chafu. Yuko kawaida. Kiingereza chake kina lafudhi hakika ya Kiafrika.  Mpakistani kamwambia hana hiyo paundi moja ambayo ni kama ya shilingi elfu mbili na kitu za Tanzania.
“Nipe bwana nitakurudishia!” Jamaa kazoza, na kusonya juu.
Hapo sasa ananizonga na miye maana kanafasi tulichosimama wawili hakitutoshi. Kawaida huku Uzunguni mteja anapokuwa akihudumiwa, wale wanaomfuata  husubiri zamu yao katika foleni. Hivyo jamaa hajafuata utaratibu. Ongeza kiburi.
Mpakistani kapokea fedha niliyompa. Akaiweka kibindoni. Upesi akachakura  makabrasha nyuma ya bidhaa zake, akarejea na chupa ndogo ya maji. Akampa jamaa. Bure.
“Haya chukua, maji. Hela sina, samahani.”
Ombaomba si kapewa maji aliyotaka? Sasa...
Sasa...kwani atayapokea kwa shukrani?
“Hayo siyo maji niliyohitaji. Nataka yenye gesi. Koo langu haliko sawa. Nipe yenye gesi bwana!”
“Sina yenye gesi. Samahani!” Bado mwenye duka anampa jamaa chupa ya maji.
Mwafrika mwenzangu  si kaja juu?
Akasonya. “Nakuomba basi unipe paundi moja. Paundi moja tu. Nikatafute maji. Koo langu kavu. Nina mafua. Hii baridi inanimaliza. Nitakurudishia!” Mimi sasa narejeshewa simu yangu. Najitayarisha kuondoka.
Mpakistani kafura.
 “Samahani sana!...” ....Kaanza.
 Tukumbushane mila na desturi. Neno samahani, yaani “sorry,” kwa Waingereza ni muhimu sana. Utamaduni na kauli yao  wenyeji hawa waliotutawala zamani,  inakusihi ulijue, ulimanye,  ulithamini.  Samahani yaani Sore, ni neno doooogo  unapashwa kulikariri, kulikumbuka, kulitaja, kuliheshimu. Ukikanyagwa. Ukikanyaga. Ukipigwa kikumbo. Ukigonga kikumbo.  Ukiomba, ukiombwa, ukikataa,  ukikubali; ukikosea, ukikosewa. Kwa Mwingereza hufunga mashtaka na kuondoa kisirani na kutoelewana. Ni kama sisi kumpa mwenzio pole. Amefiwa, amekukosea, umemkosea; kaugua, umeugua. Na kadhalika.
“Samahani, “ akaanza Mmachinga. “Hili hapa ni duka. Siwezi kuwa nagawa hela kwa kila mtu. Biashara hii.  Si kanisa au msikiti. Nimekupa maji hutaki. Nifanyeje?”
Mwafrika (maana nilikadiria lafudhi yake nzito ni Mmatumbi mwenzangu) pandikizi la mtu, akapiga kite, akapandisha mabega, akasonya mara ya tatu, akafutua mdomo; akatoa kidole cha shahada alichomnyooshea, kikunguru, kijana wa Kipakistani.
“Yaani nakuomba  paundi moja tu unanikatalia? Nipe bwana nitakurudishia! Nyinyi watu sijui kwanini mna roho mbaya namna hii? Wabinafsi...”
Niliwahi kuandika kuwa  wenye maduka huwa hawapotezi muda kujibishana. Huyu kakaa kimya. Alikuwapo mteja mwingine anatusubiri nyuma ya mstari.
“Naweza kukusaidia? ....”
Mteja akahudumiwa. Akalipa. Akayeyuka.
Wakati akiondoka, yule Mmatumbi mwenzangu, kero inamtafuna, utadhani utitiri wa kuku, sasa anatingisha kichwa akitukana kikwao. Matusi. Misonyo. Huyoooo...hamsini.
Mmachinga akanigeukia.
“Unaona? Sisi  tunafanya kazi usiku na mchana wengine wanakuja kututukana?”
Naam.  Hawa Wahindi na Wapakistani wanachukiwa sana na baadhi ya watu weusi. Ukweli nafasi za biashara zipo kila mahali.  Bora ujue utaratibu. Jamii ya kibepari hii. Ukitaka cha mvunguni, chutama. Walihamia walipofukuzwa  Uganda na marehemu Idi Amin mwaka 1971 na 1972. Wengine mathalan huyu Mmachinga, wamefuata ndugu zao waliohamia miaka 50 au 60 iliyopita toka bara Asia. Wapo waliokuja kusoma wakazamia. Nidhamu. Alfajiri hadi magharibi. Iwe Jumapili sikukuu ya Idd El Fitr, Krismasi, mapumziko ya kiserikali. Wamo kazini.  Hawajui kudorora. Weka sasa ushirikiano baina yao. Hujengana. Sisi? Kusengenyana. Kulogana.  Kutaka vya bure.
  Wiki iliyopita tulizungumzia yanayoendelea Nigeria. Bajeti ya ulinzi wa kitaifa,  ni kali kuzidi majeshi mengi barani. Lakini “wameshindwa” (kama kweli ni kushindwa) kupambana na waasi wanaoteketeza makazi na kuua  wanawake, watoto  wa shule na maskini. Hapo hapo viongozi wanaomba msaada kwa Wazungu. Neno gani ndugu msomaji tutumie kuiita hulka, mwenendo, msimamo na tabia hii ya baadhi ya wanasiasa wetu Afrika?
Share on :
 
Copyright © 2015 Raizoni Blog
Distributed By My Blogger Themes | Design By SPARTO Inc Team