
Hata hivyo baadhi ya athari hizo zinawakumba
vijana ambao ndiyo kundi kubwa la Watanzania moja ikiwa kupata hofu ya
kuamua kutekeleza au kuamua mambo mbalimbali ikiwamo kufunga ndoa.
Tatizo hilo ni ukweli unaowekwa hadharani na
maelezo mbalimbali ikiwamo takwimu za kitaalamu za Sensa za Idadi ya
Watu na Makazi iliyofanyika nchini mwaka 2012, iliyobainisha kuwa
asilimia ya watu waliooa au kuolewa imepungua.
Taarifa za msingi za kidemografia, kijamii na
kiuchumi ya matokeo muhimu yaliyojitokeza kwenye Sensa ya Watu na Makazi
ya mwaka 2012 zinaonyesha kwamba asilimia ya watu waliooa au kuolewa
imepungua.
Takwimu za Sensa
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya
Taifa ya Takwimu (NBS) na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali
(OCGS),Zanzibar hali hiyo inaweza kuwa imesababishwa na ugumu wa maisha
na ugonjwa wa Ukimwi.
“Asilimia ya watu waliooa au kuolewa imepungua
kutoka asilimia 54 mwaka 2002 hadi asilimia 51 mwaka 2012. Hii inaweza
kuwa imesababishwa na ugumu wa maisha na athari za ugonjwa wa Ukimwi,”
imeeleza taarifa hiyo.
Inaeleza kuwa asilimia 58 ya watu wenye umri wa miaka 15 na zaidi nchini wameoa au kuolewa au kuishi pamoja na wenzi wao.
Matokeo hayo muhimu yanabainisha kwamba idadi ya
watu walioachana au kutengana imepungua kutoka asilimia tano mwaka 2002
mpaka asilimia nne mwaka 2012, hali ambayo ilielezwa kuwa ni ishara ya
kudumu kwa ndoa kadiri miaka inavyoongezeka.