
Dar es Salaam. Mbio za urais ndani ya CCM sasa zimefikia pabaya baada ya kuibuka hofu ya kuwapo kwa mpango wa kuivuruga Kamati Kuu kabla ya haijakutana kuchuja majina ya makada watakaotakiwa kupigiwa kura na Halmashuri Kuu ili kumpata mgombea atakayepeperusha bendera ya chama hicho kwenye Uchaguzi Mkuu.
Hadi sasa CCM haijatangaza ratiba yake kwa ajili ya kuongoza wanachama wanaotaka kuwania uongozi wa ngazi mbalimbali kwa tiketi ya chama hicho.
Hata hivyo, Mwananchi ilitaarifiwa wiki hii kuwa
Kamati Kuu ya CCM itakutana Mei 20 na kufuatiwa na vikao vya siku mbili
vya Halmashauri Kuu Mei 21 na 22 kwa ajili ya kupitisha ratiba, ilani na
taratibu nyingine za uchaguzi, ikiwa ni kuashiria kuanza rasmi kwa
mchakato wa uchaguzi ndani ya chama hicho kikongwe.
Wakati chama kikitafakari kuanzisha rasmi mchakato
wa uchaguzi, tayari kuna habari kuwa moja ya makundi ya makada
wanaowania urais limeonyesha kutokuwa na imani na mwenendo wa Kamati Kuu
ambayo ina jukumu la kuchuja wanaowania urais na kupeleka majina
Halmashauri Kuu kwa ajili ya kupigiwa kura.
SOURCE: Mwananchi
SOURCE: Mwananchi